>

HUYU HAPA AMEANDALIWA NA SIMBA KUIMALIZA YANGA

MENEJA wa Habari wa Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally amesema wamempa jukumu mshambuliaji wao tegemeo Mzambia Moses Phiri la kuwalipua watani wao wa jadi, Yanga.

Hiyo ni katika kuelekea mchezo wa raundi ya Kwanza ya Ligi Kuu Bara ambao utapigwa kesho Jumapili kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar.

Mchezo huo muhimu kwa kila timu, Yanga kurejesha imani ya mashabiki wao baada ya kuondolewa katika hatua ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika huku Simba ikitaka kulipa kisasi cha kufungwa mara mbili Ngao ya Jamii.

 Ally amesema kuwa mshambuliaji huyo ameahidi kupiga saluti mara baada ya kuwafunga watani wao, Yanga katika mchezo huo.

Ally amesema kuwa mshambuliaji huyo hakuwa sehemu ya kikosi cha timu hiyo, kilichocheza mchezo wa Ngao ya Jamii katika msimu huu ambao ulimalizika kwa Yanga kushinda mabao 2-1 yote yakifungwa na Mkongomani, Fiston Mayele.

Aliongeza kuwa uwepo wa mshambuliaji huyo kutaimarisha safu nzuri ya ushambuliji huyo ambaye ameahidi kufunga bao katika mchezo huo.

“Phiri hakuwa sehemu ya wachezaji waliocheza mchezo uliopita wa dabi ambao ulikuwa wa Ngao ya Jamii uliomalizika kwa Yanga kushinda mabao 2-1.

“Lakini katika dabi hii atakuwepo na ameahidi kupiga saluti mara baada ya kuwafunga Yanga katika mchezo huo ambao wa umuhimu kwetu, na moja ni kuendelea kukaa kileleni na pili kuendelea na shangwe za furaha baada ya kufuzu makundi kimataifa.

“Nafahamu haitakuwa rahisi, lakini ninaamini atapambana na kufanikiwa kufunga katika mchezo huo baada ya kuwakosa Yanga katika Ngao ya Jamii uliopita,” amesema.