CRDB YAFUNGUKA SAKATA LA YANGA ‘HAWADAIWI CHOCHOTE’

WADHAMINI wa mashindano ya FA, Bank ya CRDB imetoa ufafanuzi kuwa ilishafanya malipo yote ya msimu uliopita katika Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), hivyo wao hawadaiwi kitu chochote.

Ikumbukwe kwamba msimu wa 2023/24 mabingwa wa taji hilo walikuwa ni Yanga SC walioshinda kwenye fainali mbele ya Azam FC kwa ushindi wa penati 6-5. Azam FC ni Idd Nado alikosa penati kwenye mchezo huo.

Ni 02/06/2024 mchezo huo wa kufunga msimu ulichezwa kwa wababe hao wawili kukutana na Yanga SC chini ya Miguel Gamondi ilitwaa ubingwa huo ikiwa ni mara ya nne kutwaa taji hilo baada ya kuingia fainali nne mfululizo.

Ni fainali ya tano Yanga SC imeingia ambapo mchezo wao ujao unatarajiwa kuchezwa dhidi ya Singida Black Stars, Uwanja wa New Amaan Zanzibar ambapo Yanga SC wamebainisha kuwa hawatacheza mchezo huo mpaka walipwe hela ya ubingwa wa msimu uliopita.

Kupitia kwa Ofisa Habari wa Yanga SC, Ali Kamwe aliweka wazi kuwa miongoni mwa matakwa yao manne kwenye kucheza mchezo wa Kariakoo Dabi dhidi ya Simba SC ni kulipwa hela ya ubingwa wa CRDB Federation Cup msimu uliopita.

Taarifa rasmi iliyotolewa na CRDB imeeleza kuwa tayari ilishakamilisha malipo hayo kwa wakati baada ya mshindi kupatikana.

Taarifa hiyo imeeleza namna hii:-“Malipo yote ya msimu uliopita yalifanyika kwa TFF, kwa mujibu wa mkataba baina ya Bank na TFF, hivyo kama wadhamini hatudaiwi chochote, ikiwemo malipo ya msimu uliopita.
“Malipo yote ya msimu uliopita yalifanyika kwa TFF, kwa mujibu wa mkataba baina ya Bank na TFF,” ilisema taarifa ya CRDB Bank.