>

WAKIMATAIFA KAZINI SEPTEMBA

WAKIMATAIFA katika Ligi ya  Mabingwa ambao ni Yanga chini ya Kocha Mkuu Miguel Gamondi watakuwa na kazi ya kusaka ushindi wakiwa nyumbani kusaka tiketi ya kutinga hatua ya makundi.

Ikumbukwe kwamba kwenye mchezo uliopita wakiwa ugenini ubao ulisoma CBE SA 0-1 Yanga bao la ushindi likifungwa na Prince Dube dakika ya 45 akitumia pasi ya Aziz Ki.

Mchezo ujao kimataifa kwa Yanga watakuwa Uwanja wa New Amaan Complex dhidi ya CBE SA ambapo tayari timu imerejea Bongo kwa maandalizi ya mwisho kuelekea mchezo huo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa saa 2:30 usiku kwa kila timu kusaka ushindi ndani ya uwanja huku Yanga wakiwa wametanguliza mguu mmoja kutinga hatua ya makundi.

Jumamosi Yanga wakimaliza kazi yao kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba itakuwa kwenye Kombe la Shirikisho, Uwanja wa Mkapa itakuwa dhidi ya Al Ahly Tripoli ya Libya.

Ipo wazi kwamba kwenye mchezo uliopita ugenini baada ya dakika 90 ubao ulisoma Al Ahly Tripoli 0-0 Simba hivyo mshindi kwenye mchezo wa Jumapili atafungua ukurasa wake kutinga hatua ya makundi kimataifa.

Imeandikwa na Lunyamadzo Mlyuka, Dizo Click