>

SIMBA YAWAFUATA WAPINZANI KIMATAIFA KAMILI, KUPITA UTURUKI

KIKOSI cha Simba kinachonolewa na Kocha Fadlu Davids  mapema Septemba 11 kimekwea pipa kuelekea Libya kwa ajili ya maandalizi ya mwisho mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Ahli Tripoli ya Libya wakiwa kamili gado.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Septemba 15 ambapo Simba wataanza ugenini na kurejea kwenye mchezo wa pili Uwanja wa Mkapa.

Ahmed Ally, Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano Simba amesema kuwa kila kitu kinakwenda sawa kwa upande wa mpangilio wa safari yao ya Septemba 11 kuelekea Libya ambapo watapitia Uturuki.

“Tunakwenda kucheza na wapinzani wetu ambao sio wa kuwabeza tupo tayari kwa kazi na msafara utapita Uturuki hiyo ujue ni Ulaya baada ya hapo tutaunganisha safari kuelekea Libya kwa ajili ya mchezo wetu wa Kombe la Shirikisho.

“Wachezaji wengine ambao wapo kwenye timu ya taifa wale ambao wapo nchini Ivory Coast ambao kutakuwa na mchezo kati ya Tanzania dhidi ya Guienea wao wataanza safari kuanzia Ivory Coast itakuwa Septemba 11 kisha watajiunga na timu.

“Wote ikifika Septemba 12 watakuwa Libya kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kuelekea mchezo wetu wa kimataifa ambao una umuhimu mkubwa kwetu Wanasimba tunahitaji kupata ushindi na tupo tayari.”

Imeandikwa na Lunyamadzo Mlyuka.