VITAL’O FC YA BURUNDI DHIDI YA YANGA KUPIGWA KATIKA UWANJA WA AZAM COMPLEX

Kwa mjibu wa Msemaji wa timu ya Vital’O FC ya Burundi, Arsene Bucuti amefahamisha kuwa mechi ya awali ya Klabu bingwa ya Afrika kati ya timu hiyo na Yanga SC itapigwa katika Uwanja wa Azam Complex majira ya saa kumi kamili alasiri wiki ijayo.

Vital’O FC ambayo ipo jijini Mwanza katika mechi ya kirafiki dhidi ya Pamba Jiji FC kwenye kilele cha Pamba Day itakwea pipa Agosti 11 kuelekea Dar es salaam kujiandaa kukipiga na Yanga SC.

Vital’O FC imesema kuwa haikwenda klabu bingwa barani Afrika kwa ajili ya kushiriki bali kufanya vyema ikiwemo kupata alama sita za kwanza dhidi ya Wananchi.

Klabu hiyo yenye historia kubwa nchini Burundi ikiwa na makombe 21 ya Ligi Kuu ilikuwa imemaliza misimu nane bila kutwa kombe hilo.