SIMBA WATAJIWA BEI YA FEISAL KUTOKA AZAM

UONGOZI wa Azam FC umekubali kumuachia kiungo wake mshambuliaji, Feisal Salum kwenda katika klabu itakayomuhitaji katika msimu ujao kwa dau la Sh 5Bil.
Kiungo huyo anatajwa katika usajili wa Simba ambayo imepanga kufumua kikosi chao na kukiimarisha ili kirejeshe makali yake msimu ujao.

Simba ndani ya misimu mitatu mfululizo imeshindwa kubeba ubingwa wa Ligi Kuu Bara ambayo yote imekwenda kwa watani wao wa jadi, Yanga.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Ofisa Habari wa Azam FC, Hasheem Ibwe alisema kuwa wapo tayari kumuachia kiungo huyo ambaye ni mshindi wa pili kwenye ufungaji akitupia mabao 19 kwenye ligi kuu kwenda kuichezea klabu nyingine kwa sharti la kufuata utaratibu wa usajili.

Ibwe alisema kuwa wamesikia tetesi nyingi za kiungo wao kuhusishwa na baadhi ya klabu za ndani na nje ya nchi ambazo zimeonyesha nia ya kumsajili hivyo wao hawawezi kumzuia lakini hiyo inayomtaka ijiandae kutoa dau la Sh 5Bil.