>

SIMBA YAZIPIGIA HESABU POINTI ZA TABORA UNITED

UONGOZI wa Simba umeweka wazi kuwa hesabu kubwa ni kupata pointi tatu kwenye mchezo wao wa ligi dhidi ya Tabora United.

Februari 6 Simba ina kibarua cha kusaka pointi tatu kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Tabora United unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi.

Tayari viingilio kwenye mchezo huo vimewekwa wazi ikiwa ni 5,000 mzunguko, VIP 10,000 huku VVIP ikiwa ni 20,000.

Ahmed Ally Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano Simba amesema wanatambua ushindani ni mkubwa hivyo wataingia kwa tahadhari kuwakabili wapinzani wao.

“Tupo tayari na timu imefika Tabora kamili kwa ajili ya mchezo wetu muhimu ambao utakuwa na ushindani na kikubwa tunahitaji pointi tatu.

“Tumetoka kupata ushindi kwenye mchezo dhidi ya Mashujaa Uwanja wa Lake Tanganyika ilikuwa kazi kweli lakini wachezaji walifanya kazi kubwa kupata ushindi,”.

Mchezo uliopita ubao wa Uwanja wa Lake Tanganyika ulisoma Mashujaa 0-1 Simba bao likifungwa na Saido Ntibanzokiza dakika ya 16 kwa mkwaju wa penalti.