>

AZIZ KI ATAJWA KICHAPO CHA KURUGENZI

KOCHA msaidizi wa Kurugenzi FC, Bernard Magogo amesema kuwa sababu kubwa iliyowavuruga wachezaji wake wakapoteza kwa kufungwa mabao 8-0 ni safu ya kiungo ya Yanga iliyokuwa inaongozwa na Aziz KI.

Desemba 11,2022 Kurugenzi FC ilikubali kupoteza mchezo wa raundi ya Pili jambo lililoifanya ikafungashiwa virago na mabingwa watetezi.

 Magogo amesema kuwa walikuwa na mbinu walizopanga kabla ya mchezo zilitibuliwa mapema baada ya kufungwa bao la kwanza.

“Tulikuwa tunajua kwamba tunakutana na timu kubwa na ngumu hivyo mipango tulipanga mapema vizuri lakini kiungo wao hasa Aziz KI huyu alihusika kwenye kutuvuruga na kusababisha kufungwa mabao yote.

“Unaweza kuniuliza kwamba hajafunga, lakini ukweli ni kwamba licha ya kutokufunga bado alikuwa anahusika kwenye kuwatengenezea nafasi wachezaji wengine na hilo lilifanya eneo la kati kushindwa kufanya kazi.

“Mwisho wa siku bao la mapema lilituvuruga pia na kwa sasa tunarudi kwenye Ligi Daraja la Pili kuendelea na kazi yetu kusaka ushindi tunaamini kwamba huko tutafanya vizuri,” amesema Magogo