>

DILUNGA AFICHUA KUHUSU SIMBA

KIUNGO Hassan Dilunga ambaye kwa sasa anajiuguza majeraha yake, amesema kuwa amekuwa akiwaambia wachezaji wa timu hiyo kupambana kuwapa furaha mashabiki.

 Nyota huyo ambaye alijiunga na Simba akitokea Mtibwa Sugar kwa sasa kandarasi yake imemeguka na hajaongezewa mkataba mwingine akiwa ni huru.

Ikumbukwe kwamba Dilunga hakutambulishwa siku ya Simba Day ambayo ilitumika kuwatambulisha wachezaji wapya na wale waliokuwa na kikosi hicho msimu uliopita.

Dilunga amebainisha kuwa amekuwa akizungumza na wachezaji wa Simba muda mwingi kila wakati kwa kuwa ni familia yake ambayo anaikumbuka.

“Ninaikumbuka familia yangu ya Simba, ninawapenda wachezaji wenzangu na huwa ninawasiliana nao kwa kuwaambia kwamba lazima wapambane kuwapa furaha mashabiki wa Simba na kutimiza majukumu yao.

“Wakati naumia mkataba wangu ulikuwa umesalia miezi miwili na sasa sijasaini dili jingine ila kuna jambo litatokea kwani mawasiliano bado yapo na Simba wamekuwa wakihusika kwenye matibabu yangu pamoja na watu wengine ambao wakiona hii watajua kwamba wanahusika,” amesema Dilunga.