KOCHA YANGA:MAYELE ATAFUNGA TU

NASREDDINE Nabi, Kocha Mkuu wa Yanga amesema kuwa mshambuliaji wake namba moja Fiston Mayele atafunga kwenye mechi zilizobaki kwa kuwa anapenda kufunga na uwezo anao.

Mayele kwenye mechi nne mfululizo za ligi hajafunga akiwa ameachwa kwa bao moja na mtupiaji namba moja George Mpole wa Geita Gold mwenye mabao 13 na pasi tatu za mabao.

 Nabi amesema kuwa suala la kufunga kwa mshambuliaji haliepukiki ila huwa kunakuwa na kipindi cha mpito kinawakuta wachezaji wote.

“Kwenye upande wa kufunga kia mmoja anajua kwamba Mayele ni ana uwezo wa kufunga na anaposhindwa kufunga haina maana kwamba hatafunga katika mechi atakazocheza atafunga tu.

“Bado kuna mechi zipo mkononi za kucheza hapo nina amini akipata nafasi atafunga na akishindwa kufunga basi atatengeneza nafasi kwa ajili ya mwingine kushinda, ambacho tunaangalia ni ushindi wa timu na sio mchezaji,” amesema Nabi.

Yanga leo itakuwa na kazi ya kusaka ushindi mbele ya Mbeya Kwanza kwenye mchezo wa ligi unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa.