Home Sports INONGA APEWA KAZI NYINGINE

INONGA APEWA KAZI NYINGINE

BEKI wa kazi chafu ndani ya kikosi cha Simba, Henock Inonga amebebeshwa zigo jipya la kazi ndani ya kikosi hicho na benchi la ufundi chini ya Kocha Mkuu,Pablo Franco.

Jukumu hilo jipya kwa sasa ni lile la kuweza kuichezesha timu na kugawa mipira kwa wachezaji wenzake kwenye mechi ambazo anacheza huku akiwa na kazi ya kuendelea kulinda lango.

Kazi hiyo ilianza kwenye mchezo dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Mkapa, Simba iliposhinda mabao 4-1 na Inonga kwenye mchezo huo aliweza kufunga bao lake la kwanza akiwa na Simba kwenye ligi.

Kipindi cha kwanza Inonga alikuwa ni beki wa kati lakini kipindi cha pili alipoingia Keneddy Juma, Inonga alikuwa eneo la kati jambo lililompa nafasi ya kuweza kufunga.

Kwenye mchezo dhidi ya Kagera Sugar,Inonga alicheza nafasi ya kiungo huku akiwa ni msambaza mipira kwa viungo wengine alioanza nao ikiwa ni pamoja na Rally Bwalya na Mzamiru Yassin.

Pablo Franco, Kocha Mkuu wa Simba amesema kuwa inamlazimu kufanya hivyo kwa kuwa wachezaji wengine ni majeruhi.

“Kiungo kama Jonas Mkude,Taddeo Lwanga hawajawa fiti kwa kuwa ni majeruhi hivyo ninapaswa kuwatumia wachezaji waliopo kuweza kucheza na kutafuta ushindi,”.

Lwanga tayari ameshaanza kucheza mechi za ushindani na alipewa dk 20 kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho hatua ya robo fainali dhidi ya Pamba SC..

Previous articleMAYELE:MABEKI WANATAKA NISIFUNGE
Next articleSAUTI:MAYELE KUTETEMA,NABI APIGA MKWARA