KMC WAIVUTIA KASI MTIBWA SUGAR

KIKOSI cha KMC FC leo Mei 9 kimeanza mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa ligi dhidi ya Mtibwa Sugar utakaopigwa Alhamisi ya Mei 12 katika Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.

Timu hiyo ya Manispaa ya Kinondoni chini ya Kocha Mkuu, Thierry Hitimana inajiandaa na mchezo huo muhimu ikiwa nyumbani na hivyo kuhitaji kufanya vizuri ikiwa ni mara baada ya kutoka kupoteza dhidi ya Azam FC katika Uwanja wa Azam Complex Chamanzi Jumamosi ya mwishoni mwa wiki.

KMC kwa sasa inahitaji kufanya vizuri katika michezo iliyosalia ili kujihakikishia kumaliza katika nafasi nzuri kwenye msimamo wa ligi kuu ya NBC licha ya kwamba ushindani umezidi kuongezeka siku hadi siku.

Ofisa Habari wa KMC, Christina Mwagala amesema:“Tunahitaji kufanya vizuri kwenye michezo yetu inayofuata, baada ya kupoteza dhidi ya Azam, tupo kwenye nafasi ambayo sio nzuri kwa sasa, lakini ubora wa wachezaji wetu pamoja na benchi la ufundi linaloongozwa na Kocha Mkuu Hitimana tunayo nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye michezo iliyobakia.

“KMC tunaendelea na mazoezi, tuna siku tatu tu za kufanya maandalizi ya mchezo mwingine dhidi ya Mtibwa Sugar, ni mchezo mgumu na wenye ushindani lakini tunahitaji kutumia vizuri uwanja wetu wa nyumbani kupata matokeo mazuri.

“Mchezo uliopita tulipoteza dhidi ya Azam tukiwa ugenini, lakini hiyo bado haituvunji moyo wala kututoa kwenye morali zaidi inatupa changamoto ya kupambana kwenye michezo mingine inayokuja kwa sasa, ligi bado haijamalizika tutajitajidi kuhakikisha kwamba tunamaliza kwenye nafasi nzuri msimu huu.

KMC ipo kwenye nafasi ya 11 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 22 na kukusanya jumla ya alama 24 ambapo mchezo dhidi ya mtibwa utakuwa wa 23.