DJUMA APEWA KAZI NYINGINE YA MAYELE NA NTIBANZOKIZA

BEKI mkongwe wa Yanga, Mkongomani, Shaaban Djuma, amepewa majukumu mapya ya kupiga penalti zote itakazozipata timu hiyo inayowaniwa ubingwa wa Ligi Kuu Bara.

Aprili 6,2022 Djuma alipiga penalti na kufunga bao la kwanza dhidi ya Azam katika ushindi wa 2-1, Chamazi.

Hiyo ni penalti ya pili kwa beki huyo kuipiga katika msimu huu tangu ajiunge nayo akitokea AS Vita ya Congo, Kinshasa. Awali penalti za timu hiyo zilikuwa zikipigwa na Mrundi, Said Ntibazonkiza ‘Saido’ na Mkongomani Fiston Mayele ambaye ndiye kinara wa mabao katika ligi akifunga mabao 11.

 Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mtunisia Nasreddine Nabi alisema kuwa wachezaji wote wana viwango vya kupiga penalti, lakini amemchagua Djuma hivi sasa. Nabi alisema kuwa anamchagua mchezaji wa kupiga penalti kutokana na ubora na uwezo wake ambao anauonyesha mazoezini.

Aliongeza kuwa beki huyo ataendelea kupiga penalti zote zitakazopatikana wakati akiwa uwanjani kwa kuanzia michezo ya ligi na Kombe la Shirikisho la Azam Sports.

“Djuma anafanya vizuri mazoezini katika programu ya kupiga penalti ambayo ipo katika mazoezi ya kila siku.

“Tofauti na Djuma wapo wachezaji wengine wengi wenye uwezo huo wa kupiga penalti, lakini kwangu Djuma ndiye anayefanya vizuri hivi sasa.

“Hivyo ataendelea kupiga katika michezo ya ligi na michuano mingine tutakayoshiriki katika msimu huu ambao ni mzuri kwetu,” alisema Nabi.

Chanzo:Championi.