>

BEKI MTIBWA SUGAR AINGIA ANGA ZA SINGIDA BIG STARS

BAADA ya kuwaaga mabosi wake Mtibwa Sugar beki wa kazi Nickson Kibabage anatajwa kuwa kwenye rada za kuibukia ndani ya Singida Big Stars.

Nyota huyo aliwaaga wachezaji na viongozi wake rasmi Desemba 13 kwa kueleza kuwa anashukuru kwa muda wote ambao alikuwa ndani ya timu hiyo.

Pia alikuwa anavaa kitambaa cha unahodha jambo ambalo liliwafanya Mtibwa Sugar kujivunia kijana huyo kuwa kiongozi mbele ya wachezaji wenzake uwanjani.

Mbali na Singida Big Stars nyota huyo ambaye anacheza nafasi ya beki wa kushoto anatajwa kuwa amepata ofa nyingine nje ya nchi.

Ikumbukwe kwamba mzawa huyo alirejea ndani ya Mtibwa Sugar akitokea KMC.

Licha ya kucheza nafasi ya beki nyota huyo alikuwa anacheka na nyavu ambapo katupia mabao matatu kati ya 21 ambayo yamefungwa na timu hiyo.