YANGA YATHIBITISHA KUTOSHIRIKI MCHEZO DHIDI YA SIMBA HADI MATAKWA YATIMIZWE

Klabu ya Yanga Sc imethibitisha kuwa mnamo Juni 7, 2025 ilipokea barua kutoka Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kwa ajili ya kuhudhuria kikao maalum cha kujadili masuala yahusuyo mchezo namba 184 wa Ligi Kuu ya NBC, YANGA dhidi ya Simba na kubainisha kuwa uongozi wa klabu hiyo umetii wito huo.

Taarifa ya leo Juni 9, 2025 iliyotolewa na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo imeeleza kuwa uongozi wa klabu hiyo umeshiriki kikao hicho kilichofanyika leo kwenye ofisi za Bodi ya Ligi Tanzania zilizopo jengo la NSSF Mafao House, Dar Es Salaam, kuanzia saa 4:00 asubuhi na kubainisha kuwa imewasilisha msimamo wake kuwa haitashiriki mchezo huo mpaka pale matakwa yao yatakapotimizwa

“Baada ya majadiliano ya saa kadhaa, Viongozi wa Klabu waliwasilisha msimamo wa Klabu YETU kuwa hatutashiriki mchezo namba 184 uliopangwa kufanyika tarehe 15 Juni 2025 mpaka pale matakwa yetu tuliyoyawasilisha kwa maandishi kwao yatakapotimizwa.” — imesema sehemu ya taarifa hiyo.

“Tunawatakia kila la heri Bodi ya Ligi na Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini katika kushughulikia matakwa yetu yenye mustakabali mkubwa kwenye maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania.” — imesema Yanga Sc