>

AZAM FC YATAJA UGUMU WA APR ULIPO

BENCHI la ufundi la Azam FC limebainisha kuwa lina kazi kubwa yakufanya kuelekea mchezo wa marudio dhidi ya APR ya Rwanda unaotarajiwa kuchezwa Agosti 24 2024 huku likiweka wazi kuwa ugumu wa kupata matokeo mbele ya wapinzani wao ni eneo la ulinzi kutokana na namna ambavyo wanajipanga.

Ipo wazi kwamba mchezo wa awali wa Ligi ya Mabingwa Afrika uliochezwa Uwanja Mkapa baada ya dakika90 ubao ulisoma Azam FC 1-0 APR hivyo kazi kubwa ni kuelekea mchezo wa marudio ambao utaamua mshindi atakayesonga mbele hatua inayofuata.

Yusuph Dabo, Kocha Mkuu wa Azam FC amabeinisha kuwa ana furaha kubwa kwa kilichotokea katika mchezo wa kwanza kwa kuwa walipata matokeo hivyo wanajipanga kuelekea mchezo wa pili ugenini nchini Rwanda.

“Nina furaha kwa kilichotokea kwa kuwa tumepata matokeo na ipo wazi kwamba wapinzani wetu sio timu ya kubeza ni moja ya timu ambayo ni ngumu kufungika kutokana na namna inavyojipanga kwenye ulinzi pamoja na ubora wake.

“Lakini licha ya ugumu ambao upo watu wanapaswa kuelewa kwamba yote haya tunayachukulia kwa umakini na ambacho tunahitaji ni kwenda kupata matokeo mazuri hivyo kikubwa ni maandalizi mazuri ambayo tunayafanya.

“Tunao ubora wa kutosha wa kwenda Rwanda na kushinda ni jambo tu la kupumzika vizuri na kujiandaa vizuri kwa mchezo wa pili wiki ijayo (hii).”