>

YANGA KAMILI KUWAKABILI VITAL’O

UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa upo tayari kwa mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Vital’ O ya Burundi unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Azam Complex.

Huu ni mchezo wa awali ambapo Yanga atakuwa ugenini baada ya Vital’O kuomba kutumia Uwanja wa Azam Complex kuwa ni uwanja wake wa nyumbani.

Ali Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga amesema kuwa wanatambua umuhimu wa mchezo huo na tambo za wapinzani wao wamesikia hivyo wanakwenda kufanya kazi kwa vitendo uwanjani.

“Hatuna jambo dogo sisi na tunatambua ni mchezo muhimu kwa kila mmoja kupata ushindi lakini kwa kile ambacho wamekipanda watavuna uwanjani, tukutane Azam Complex.”

Miguel Gamondi ambaye ni Kocha Mkuu wa Yanga amebainisha kwamba benchi la ufundi lipo tayari na hesabu kubwa ni kupata matokeo kwenye mchezo wao kufikia malengo ya kusonga mbele kimataifa.