NYIE HAMUOGOPI? YANGA WANA JAMBO LAO

MWAMBA wa Lusaka Clatous Chama amesema kuwa Agosti 4 2024 wana jambo lao Uwanja wa Mkapa hivyo mashabaki wajitokeze kwa wingi.

Ni Kilele cha Tamasha la Wiki ya Wananchi ikiwa ni maalumu kwa ajili ya utambulisho wa wachezaji wapya na wale waliokuwa na kikosi hicho kinachonolewa na Kocha Mkuu, Miguel Gamondi.

Ipo wazi kwamba Chama ni ingizo jipya ndani ya Yanga alitambulishwa rasmi Julai Mosi 2024 ambapo msimu wa 2023/24 alikuwa mali ya Simba iliyogotea nafasi ya tatu kwenye msimamo na itashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.

Chama amesema: “Ni siku muhimu kwa Wananchi nipo hapa kuwaomba mjitokeze kwa wingi uwanjani kwa kuwa tuna jambo letu Uwanja wa Mkapa, Agosti 4 2024. Nyie hamuogopi?

Mbali na Chama mshambuliaji Jean Baleke alibainisha kuwa ni siku ya utambulisho kwa wachezaji wapya na wale ambao walikuwa kwenye kikosi hicho msimu uliopita hivyo sio kitu cha kukosa.

“Ni siku muhimu kwa Wananchi kwani kuna wachezaji wapya wamekuja na wengine bado hamjawatambua hivyo sio ya kukosa kabisa hii.”.

Kwenye Wiki ya Wananchi, Agosti 3 2024 ilikuwa ni SportPesa Supu Day ambapo wadhamini wa Yanga walihusika kwenye mpango mzimakuhakikisha mashabiki wote wanapata supu.