>

INGIZO JIPYA YANGA LIMEANZA NA ZALI HILI, CHAMA ANAKUJA

INGIZO jipya ndani ya kikosi cha Yanga, Jean Baleke ameanza kwa zali la kufunga kwenye mchezo wake wa kwanza akiwa na uzi wa njano na kijani.

Nyota huyo aliwahi kucheza ndani ya kikosi cha Simba msimu wa 2022/23 ambapo alifunga mabao 8 na msimu wa 2023/24 alipofunga mabao 8. Jumla ni mabao 16 alifunga akiwa Msimbazi.Alikutana na Thank You kwenye dirisha dogo.

Kwenye msafara wa Yanga ulioibukia Afrika Kusini Baleke alikuwa miongoni mwao huku Ofisa Habari wa Yanga, Ali Kamwe akiweka wazi kuwa watafanya utambulisho maalumu kwa ajili ya mchezaji wao mpya.

Julai 20 kwenye mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Augsburg alipata nafasi ya kucheza na kufunga bao la kwanza kwenye mchezo huo akianza na zali la kufunga.

Baada ya dakika 90 ubao ulisoma Yanga 1-2 FC Augsburg. Bao la Baleke alifunga dakika ya 85 kwa pigo la kichwa akiunganisha krosi ya kiungo Maxi Nzengeli.

Miongoni mwa wachezaji wapya waliopata nafasi ya kucheza kwenye mchezo huo ni pamoja na Clatous Chama ambaye ameweka wazi kuwa ulikuwa ni mchezo mzuri licha ya kukosa matokeo.

Duke Abuya kiungo wa Yanga ameweka wazi kuwa ulikuwa ni mchezo mzuri na furaha kubwa kupata nafasi ya kucheza licha ya kukosa matokeo kwenye mchezo huo.