>

AZAM FC WANA IMANI KUBWA KINOMANOMA

HASHEEM Ibwe, Ofisa Habari wa Azam FC amesema kuwa maandalizi ambayo yanafanyika kuelekea msimu ujao yanawapa nguvu ya kuamini kwamba watafanya vizuri kwenye mashindano ambayo watashiriki.

Azam FC inanolewa na Kocha Mkuu,Yusuph Dabo imeweka kambi Morocco kuelekea msimu mpya unaotarajiwa kuanza Agosti 16 2024 na ratiba ya Ngao ya Jamii tayari imeshatoka.

Ngao ya Jamii itaanzia hatua ya nusu fainali ikiwa ni mechi maalumu kuelekea ufunguzi wa msimu. Azam FC iliyogotea nafasi ya pili kwenye msimamo itamenyana na Coastal Union katika hatua ya nusu fainali na mshindi wa mchezo huo atakutana na mshindi wa mchezo kati ya Yanga na Simba.

Ipo wazi kwamba Simba walitwaa taji la msimu wa 2023/24 kwenye fainali iliyochezwa Mkwakwani, Tanga na Azam FC alipata ushindi wa tatu.

Wakiwa kambini Morocco Azam FC Julai 19 2024 walicheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa na mwisho ilikuwa Azam FC 3-0 US Mansour. Mabao yakifungwa na Sidibe, Sillah na Blanco wote walitupia bao mojamoja.

Ibwe amesema “Furaha kubwa kwa wachezaji kuzidi kuimarika na kupata ushindi kwenye mchezo wetu wa kirafiki hayakuwa malengo makubwa lakini imetokea. Kikubwa ni kuona tunazidi kuwa imara na tayari kwa mashindano ya msimu mpya.”