>

JKT QUEENS YAKUTANA NA RUNGU HILI

MABINGWA watetezi Ligi Kuu ya Wanawake (WPL), JKT Queens wamekumbana na rungu la faini ya  milioni 3 pamoja kupokwa pointi tano kutokana na kitendo cha kushindwa kutokea kwenye Uwanja wa Azam Complex, kuvaana na Simba katika mfululizo wa mechi za ligi hiyo.

Mechi hiyo hiyo ilikuwa ipigwe Januari 9, mwaka lakini JKT haikwenda Chamazi, kwa madai inajua mechi inachezwa Meja Jenerali Isamuhyo, huku viongozi wa klabu hiyo wakisisitiza hawakuwa na taarifa ya kuhamishwa kwa uwanja, kitu ambacho kimekanushwa na Kamati ya Soka la Wanawake ya Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) kupitia taarifa iliyotolewa jana baada ya kikao.

Taarifa ambayo imetolewa na TFF imeeleza kuwa  JKT ilikuwa inajua mechi hiyo inapigwa Azam kwani walijulishwa kikao cha kabla ya mechi kilichofanyika siku moja kabla ya tarehe ya mchezo, na kwa kuvunja kanuni ya 32.1-3 ya Ligi ya Wanawake, maafande hao wamepokwa pointi tano na kupoteza mchezo huo ambao Simba inafaidika kwa kupata pointi tatu na mabao matatu.

Mbali na kupokwa taarifa hiyo inasema imetoza fainali JKT faini ya Sh3 milioni na kumfungia pia Katibu Mkuu wa timu hiyo, Duncan Maliyabwana akifungiwa mwaka mmoja kujihusisha na masuala ya michezo.

Kutokana na maamuzi hayo, JKT iliyokuwa kileleni imeporomoka ilipokuwa na pointi 21 kwenye msimamo wa ligi ambao ushindani wake ni mkubwa.

Alliance Girls nao pia wamepokwa pointi tatu kwa kosa la kumchezesha mchezaji ambaye alikuwa hajakidhi vigezo mchezo dhidi ya Geita Gold na pointi tatu zimekwenda kwa Geita Gold.