YANGA YAPIGA MKWARA KUHUSU USAJILI

UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa kwa usajili ambao wameufanya watawasumbua kwelikweli wapinzani wao kwenye mechi zote za ushindani.

Ni mzawa Nickson Kibabage kutoka Singida Fountain Gate huyu ametambulishwa ndani ya kikosi cha Yanga kiachonolewa na Kocha Mkuu Miguel Gamondi.

Mwingine ni Jonas Mkude ambaye alikuwa ndani ya Simba sasa atakuwa ndani ya kikosi cha Yanga  Fred Gift huyu ni beki wa kati kutoka SC Villa ya Uganda naye ni mali ya Yanga.

Inatajwa kuwa tayari Yanga imemalizana na Maxi Nzengeli Mpia raia wa DR Congo huyu ni winga kutoka Maniema FC,

Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe alisema kuwa usajili umekamilika kwa viongozi waliopata kuona majina ya wachezaji wapya wamekubali.

“Kutokana na usajili makini ambao tumefanya tutawasumbua kwelikweli wapinzani wetu kwani itakuwa ni mwendo wa kuwapa furaha mashabiki na hilo lipo wazi wale waliochungulia usajili wetu wamekubali.

“Ni wachezaji bora ambao wanakuja kuongeza ule ubora wa kikosi tuliokuwa nao hivyo ni muda wa Wananchi kuendelea kufurahia kwani msimu wa 2022/23 tumefanikiwa kutwaa mataji matatu bado tunahitaji kuwa na mwendelezo bora,” amesema Kamwe.