>

SIMBA NDANI YA DAR,HESABU ZIPO HIVI

KIKOSI cha Simba chini ya Kocha Mkuu, Roberto Oliveira kimerejea salama salmin Dar kwa ajili ya maandalizi ya mechi za Ligi Kuu Bara.

Timu hiyo imebakiza mechi tatu ndani ya ligi baada ya kucheza mechi 27 na kukusanya pointi 64.

Vinara wa ligi ni Yanga ambao wao kibindoni wana jumla ya pointi 71 nao wana mechi tatu pia mkononi.
Timu hiyo imetoka kuondolewa kwenye hatua ya nusu fainali ya Azam Sports Federation.

Ni Azam FC walikuwa wababe wao baada ya dakika 90 ubao wa Nangwanda Sijaona kusoma Azam FC 2-1 Simba.

Bao la Simba lilifungwa na Sadio Kanoute ambaye mikato yake ya kimyakimya ilimfanya aonyeshwe kadi mbili za njano na kupewa kadi nyekundu.

Yale ya Azam FC yalifungwa na Lusajo Mwaikenda na Prince Dube aliyefunga bao hilo akitokea benchi.

Azam FC inasubiri mshindi kati ya Singida Big Stars dhidi ya Yanga kucheza nao fainali.