YANGA YASOGEZEWA UBINGWA

LICHA ya kikosi cha Yanga kutinga kwa mara ya kwanza hatua ya robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, lakini bado timu hiyo imepewa nafasi ya kulibebe taji hilo msimu huu.

 

Yanga imeshafuzu hatua ya robo fainali baada ya kuongoza Kundi D kwa kukusanya pointi 13, huku jana Jumatano droo ya hatua ya robo fainali ikipangwa, hivyo Yanga imeshamfahamu mpinzani wake.

Spoti Xtra limefuatilia kwa karibu kufahamu yale yanayojiri katika michuano hiyo na kubaini kwamba kikosi cha Yanga kimepewa nafasi ya nne ya kutwaa ubingwa wa michuano hiyo kati ya timu nane ambazo zimefuzu robo fainali.

Katika maoni hayo yaliyotolewa kupitia jarida kubwa la michezo barani Afrika linalofahamika kama Afirica Soccer, limeipa Yanga asilimia 14 za kutwaa kombe hilo wakiwa wanashika nafasi ya nne kati ya timu nane.

Pyramids kutoka Misri, ndio waliopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa wakiwa wanaongoza kwa kupewa asilimia 23, wakifuatiwa na AS Far Rabat ya Morroco wenye asilimia 20, huku nafasi ya tatu wakiwa US Monastir ya Tunisia wenye asilimia 15. Monastir walimaliza nafasi ya pili nyuma ya Yanga.

Yanga wakiwa na asilimia 14, ASEC Mimosas (13), USM Algers (9), Rivers (4) na Marumo Gallants (2).