>

YANGA HAWA HAPA NDANI YA DAR, AHADI KAMA ZOTE

MSAFARA wa Yanga umewasili leo Dar ukitokea Mali ulipokuwa na mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Real Bamako ambao ni wa hatua ya makundi.

Katika mchezo huo Yanga iligawana pointi mojamoja kwa ubao kusoma Real Bamako 1-1 Yanga baada ya dakika 90.

Ni Fiston Mayele alipachika bao kwa upande wa Yanga kwenye mchezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa.

Sare hiyo imewapa pointi moja na kufikisha jumla ya pointi nne ikiwa nafasi ya pili kwenye msimamo wa kundi.

Baada ya kuwasili Yanga wamekabidhiwa zawadi ya fedha ikiwa ni ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Tanzania, kwa kila timu kwenye hatua ya kimataifa ikifunga bao yeye atanunua kwa milioni.

Kupitia ukurasa wa Yanga wameandika:”Tumepokea zawadi ya kiasi cha Tsh Milioni 5 kutoka kwa Rais wetu, Mh. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa goli moja tulilofunga ugenini kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho la CAF dhidi ya Real Bamako na kufanikiwa kupata sare ya bao 1-1.

“Tunakuahidi Mama, Jumatano ya Tarehe 8/3/2023 tunakwenda kupambana zaidi na utafurahi,”.