AZAM FC YAJIVUNIA POINTI ZAO ZA KARIAKOO

UONGOZI wa Azam FC umeweka wazi kuwa umezifungia pointi za vigogo wa Kariakoo,Yanga na Simba za mzunguko wa kwanza wanasubiri nyingine.

Azam chini ya Kali Ongala imekuwa na mwendo bora ambapo kwenye mechi 8 mfululizo ilisepa na pointi 24 imeanza mzunguko wa pili kwa sare ya kufungana mabao 2-2 dhidi ya Kagera Sugar.

 Ofisa Habari wa Azam FC,Hasheem Ibwe alisema kuwa wanatambua kuhusu wapinzani wao wakubwa ndani ya tatu bora lakini wamechukua pointi mbele yao.

“Hao Yanga kwao tulichukua pointi moja na tulishinda mbele ya Simba hivyo tuna pointi nne za watani wa jadi ambao tunapambana nao kusaka ubingwa.

“Kabatini pale Azam tumechukua pointi nne hivyo hatuna mashaka tunawasubiri kwenye mzunguko wa pili wana pointi zetu tunaamini kwamba mwendo utakuwa uleule ambao tulimaliza mzunguko wa kwanza kwa ushindi.

“Wale ambao wanatubeza tutakutana nao uwanjani halafu tutawaonyesha kwa vitendo hatuna mashaka kila kitu kipo kwenye mpangilio wake mashabiki wazidi kuwa pamoja nasi,” alisema Ibwe.