>

YANGA NA AZAM FC KAMILI KUVAANA KWA MKAPA

TAMBO zimetawala kwa makocha wa Yanga na Azam FC kuelekea kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara unaotarajiwa kuchezwa kesho Septemba 6,2022 Uwanja wa Mkapa.

Yanga inayofundishwa na Kocha Mkuu, Nasreddine Nabi itakuwa nyumbani kwa mara ya kwanza msimu wa 2022/23 baada ya kucheza mechi mbili ikiwa ugenini.

Ilikuwa mchezo dhidi ya  Polisi Tanzania,ambapo ubao ulisoma Polisi Tanzania 1-2 Yanga na ule wa pili Coastal Union 0-2 Yanga yote ilichezwa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.

Kwa upande wa Azam FC wao walicheza mechi mbili chini ya Abdi Moallin ambaye amebadilishwa majukumu yake na ilikuwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar na sare ya kufungana bao 1-1 dhidi ya Geita Gold.

Nabi amesema kuwa wanatambua mchezo utakuwa na ushindani mkubwa watajitahidi kupata matokeo.

“Tunatambua Azam FC ni timu imara na ina wachezaji wazuri tutajitahidi kuweza kupata matokeo kwenye mchezo wetu ili kupata ushindi,”.

Kali Ongala, Kocha wa Azam FC ambaye yeye anawanoa washambuliaji wake wakiongozwa na Prince Dube amesema wanatambua Yanga ni timu bora watajitahidi kuwa bora nao pia.

“Tutajitahidi kuwa bora na imara kwenye kila idara ili kupata matokeo, kwa maandalizi ambayo tumefanya tunahitaji ushindi kwani wachezaji wapo tayari,” .