YANGA KUSAJILI MAJEMBE MANNE

HAJI Manara, Ofisa Habari wa Yanga amesema kuwa wamepanga kuongeza wachezaji wanne ama watatu wa kimataifa kwa ajili ya msimu ujao wa 2022/23.

 Manara ameweka wazi kuwa kuna baadhi ya nyota kadhaa wanaocheza soka katika Ligi ya Afrika Magharibi, Ligi ya Afrika Kusini, Ligi ya Angola na nyota wa Kimataifa aliyewahi kucheza soka la kulipwa Ligi ya Afrika Mashariki.

Mpango mkubwa wa Yanga ni kuweza kuboresha kikosi hicho kwa ajili ya msimu ujao wakiwa na uhakika wa kuweza kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuwa wana nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa wa ligi.

Kwenye msimamo Yanga ipo nafasi ya kwanza ikiwa na pointi 64 baada ya kucheza mechi 26 huku mabingwa watetezi Simba wakiwa nafasi ya pili na pointi 51 baada ya kucheza mechi 25.

Manara amesema:”Wanayanga waondoe hofu tayari tumekamilisha usajili wa wachezaji nyota wanne wa kigeni kwa ajili ya msimu ujao na wachezaji hawa wanakuja kwa ajili ya michuano ya kimataifa,” amesema.

Miongoni mwa wachezaji ambao Yanga inatajwa kumalizana nao ni pamoja na Aziz Ki wa ASEC Mimosas.