KOCHA NABI AIGOMEA SIMBA,HESABU KWA NAMUNGO

KOCHA Mkuu wa Yanga Mtunisia, Nasreddine Nabi amewapiga mkwara mastaa wake kwa kuwataka kutofikiria mchezo wa Dabi ya Kariakoo na badala yake kuhamisha akili zao dhidi ya Namungo FC.

Yanga kabla ya kuvaana dhidi ya Simba Aprili 30, mwaka huu katika Dabi ya Kariakoo  watacheza dhidi ya Namungo Aprili 24, katika mchezo wa ligi kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.

Timu hiyo tayari ipo kambini tangu wiki iliyopita ikijiandaa na michezo ya ligi ambao wiki iliyopita walifuzu hatua ya Robo Fainali ya Kombe la FA kwa kuwaondoa Geita Gold kwa njia ya penalti.

Yanga iko kwenye maandalizi kambini Kijiji cha Avic Town, Kigamboni nje kidogo ya Dar ni kwa ajili ya Namungo na siyo Simba.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Nabi alisema: “Michezo yote miwili iliyokuwepo mbele yetu ni muhimu ambayo itatupa pointi tatu kila mmoja, hivyo ngumu kwa wachezaji wangu kuudharau mchezo dhidi Namungo.

“Tunaanza na Namungo kwanza kuchukua pointi tatu, baada ya hapo wanafuatia Simba, hivyo siufikirii kabisa mchezo wa dabi kwa hivi sasa.”