>

PABLO:WACHEZAJI SIMBA WAMEKOSA HALI YA KUJIAMINI

PABLO Franco,Kocha Mkuu wa Simba amesema kuwa wachezaji wake kwa sasa wamekosa hali ya kujiamini kutokana na kushindwa kufunga kwenye mechi tatu mfululizo jambo ambalo linafanyiwa kazi.

Kwa sasa kwenye ligi Simba imekusanya pointi 25 ikiwa nafasi ya pili na imefunga mabao 14 huku Yanga ikiwa nafasi ya kwanza na pointi 35 na imetupia jumla ya mabao 23.

Pablo aliweza kushuhudia Simba ikipoteza kwa kufungwa bao 1-0 dhidi ya Mbeya City kisha ikalazimisha sare ya bila kufungana na Mtibwa Sugar na kazi yake mbele ya Kagera Sugar alishuhudia wakipoteza kwa kufungwa bao 1-0.

Kocha huyo amesema:”Kushindwa kufunga kwa wachezaji kwenye mechi zetu mfululizo kumewafanya washindwe kujiamini, unajua ukiwa unacheza unatengeneza nafasi unashindwa kufunga kwa namna yoyote kutakufanya usiwe imara.

“Lakini ambacho ninajua ni kwamba hilo ni jambo la mpira na tunalifanyia kazi, kwa mechi zetu zijazo imani yangu ni kwamba kila kitu kitakuwa sawa,” .

Simba ni mabingwa watetezi na waliweza kutwaa taji hilo msimu wa 2020/21 baada ya kucheza mechi 34 ilikusanya pointi 83.